14. SWAHILI KOLLOQUIUM (Bayreuth,
25. 27. Mai 2001)
Kusomesha Kiswahili kwa kutumia Vifaa vya Kompyuta
(Karin Geitlinger, Zurich)
Katika mada yangu ifuatayo ninayo malengo matatu. Kwanza, nataka
kuwajulisha mradi ambao tunajishughulisha nao huko Chuo Kikuu cha
Zurich. Mradi huo una lengo la kutengeneza masomo ya lugha ya
Kiswahili kwa kutumia vifaa vya kompyuta. La pili, katika mradi
huo, nitazungumzia juu ya uwezo na upungufu wa masomo haya mapya,
kulinganisha na masomo ya awali. Mwisho, nitatoa baadhi ya fikira
kuhusu jinsi vifaa hivyo vipya vinavyoweza kuunganishwa na mafunzo,
na itakavyomhusu mfundishaji kwenye utaratibu wake.
Mradi ninaouzungumzia unaitwa ALI Swahili; ni mfuasi wa
mradi mwingine uitwao ALI Akan. ALI Swahili
umeanzishwa mwezi wa Oktoba mwaka uliopita, chini ya uongozi wa Pr.
Bearth, na unaruzukiwa na Chuo Kikuu cha Zurich, Uswisi. Mradi huo
una lengo la kutengeneza kozi ya lugha ya Kiswahili kwenye CD, na
kutunga jinsi mpya ya masomo, kwa kutumia CD hiyo, pamoja na vifaa
vingine vya kompyuta, hasa mtandao.
Kozi kwenye CD imepangwa kuwa na masomo 24. Kila somo litakuwa na
sehemu tatu, yaani mazungumzo na maelezo ya utamaduni, sarufi, na
msamiati. Kila somo litakuwa na mifano ya mazungumzo kwenye filamu
au rikodi ya kusikiliza. Sampuli hizo zitakuwa msingi wa maelezo
yote yatakayofuata kwenye somo moja. Vilevile, kila sehemu itakuwa
na mazoezi yake. Licha ya hayo, CD itakuwa na makala kadhaa
zinazoeleza mada mbalimbali kwa undani zaidi. Makala hizi
zitaunganishwa na sehemu za masomo zinazohusika kwa njia ya
link'. Vilevile, njia hii ya links' itatumiwa
kuwafikisha wanafunzi kwenye sehemu za mtandao zinazohusika na mada
za masomo.
Mradi wa ALI Swahili umepangwa kumudu miaka miwili.
Tumetumia sura ya kwanza ya mradi huo kwa kutunga mpangilio wa
yaliyomo ya masomo yote, kukusanya data, hasa kupiga picha za video
na rikodi za kusikiliza, na kufanya utafiti kuhusu uwezo wa
ki-technolojia. Sasa hivi tuko kwenye sura ya pili, yaani kutunga
masomo yenyewe.
Mpaka leo hii tumemaliza sehemu mbili za somo la kwanza: sehemu ya
mazungumzo, ambayo inatoa maelezo ya matamshi na kuhusu jinsi
mbalimbali za kuamkiana na kuagana kwa Kiswahili, na sehemu ya
sarufi, ambayo ina maelezo ya dhana na istilahi ya utaratibu wa
ngeli. Nitatoa baadhi ya mifano kwenye maelezo yangu yafuatayo.
Kwanza, tuingie kwenye swala la manufaa ya mradi wetu: kuna vitabu
chungu nzima vya kufundisha Kiswahili, kwa nini basi tunatunga
masomo mengine? Sababu itakuwa wazi tukiangalia uwezekano wa chombo
tunachokitumia, yaani CD, kulinganisha na chombo cha kitabu. Kwa
maoni yangu, nafuu ya CD iko kwenye sehemu tatu, ambazo tunajaribu
kuzisisitiza kwenye mradi wetu:
| 1) |
Uwezekano wa kutumia picha hai na sauti. Ni wazi kwamba njia
bora kabisa kujifunza lugha ni kwenda kwenye nchi ambako lugha hiyo
inazungumzwa, au ijapo kufundishwa na mtu ambaye ni mzungumzaji wa
asili wa lugha hiyo. Lakini baadhi ya wakati, kwa sababu
mbalimbali, hii haiwezekani. Hivyo basi CD itatuwezesha kupunguza
tatizo hilo; yaani tunaweza kumpa mwanafunzi muktadha, ili ajifunze
lugha asilia na matumizi yake yenyewe, na siyo kwa kutumia tafsiri
ya lugha nyingine. Nitatoa mfano mmoja wa msamiati kusisitiza
dokezo hilo: tuchukue kitenzi kuna nazi. Naweza
nikamtafsiria mwanafunzi kitenzi hiki, lakini hawezi kufahamu maana
yake hasa, kwa sababu kwenye mazingira yake anayoishi, watu
hawakuni nazi. Lakini nikimwonyesha filamu ya mwanamke anayekuna
nazi, kwa kutumia mbuzi, atakuwa na dhana ambayo itakuwa sawasawa
na dhana aliyo nayo Mswahili mwenyewe akitamka kitenzi hiki
kuna nazi. Na yapo maneno mengine mengi ambayo dhana zao
zitafahamishwa kwa urahisi zaidi yakifundishwa kwa kutumia picha
hai. Na matumizi ya sauti kwenye maelezo yanafaa kwa sababu mbili:
Kwanza, yanafanya masomo yawe na uhalisi zaidi. Ya pili, yanampa
mwanafunzi mifano ya matamshi moja kwa moja, ambayo anaweza
kuitumia kwa kufanya mazoezi. Nitawaonyesha jinsi sauti
inavyopatikana kwenye somo letu: <U01maz-e07.html>. Sehemu
hii inaeleza tafauti baina ya sauti mbalimbali ambazo wanafunzi
baadhi ya wakati wanapata taabu kuzitamka sawasawa. Kwa kubonyeza
kwenye mifano yenyewe wanapata sauti hizo, mara zozote
watakazo. |
| 2) |
Sehemu ya pili ambapo chombo cha CD kinafaa kuliko kitabu ni
matumizi ya mifano hai. Kwa upande mmoja hii inaweza kutumika
kwenye maelezo, hasa maelezo ya sarufi. Inaweza kupangwa ili
msomaji apate umuhimu wake hatua kwa hatua, kwa kuchunguza
mwenyewe; yaani, tunamtaka mwanafunzi ashiriki kwenye kujipatia
ujuzi, siyo akae tu asome. Kwenye kozi yetu tunatumia sana rangi
kuongeza uhai wa maelezo na mifano yake; kwa kusukuma kipanya,
mwanafunzi anaweza kupeleleza undani wa mifano, na uhusiano baina
ya maelezo na mifano. Mifano miwili ifuatayo, kutoka somo letu,
inaonyesha sifa ya uhai inavyotumilika: <U01maz-e33.html>
Mfano wa kwanza unatoka kwenye maelezo juu ya maamkio. Inaelezwa
kwamba maamkio yana sehemu nne mbalimbali. Kwa kusukuma kipanya,
inawezekana kupata wazi mgawanyo baina ya sehemu hizo na sehemu za
mazungumzo yanayohusika. Mfano wa pili unatoka sehemu ya sarufi:
<U01sar-e17.html>. Hapa mwanafunzi anapewa maelezo ya
umilikifu wa ngeli nomino kwenye sentensi. Baada ya kubonyeza na
kupata mifano, anaweza kuona viambishiawali vya ngeli kwa kusukuma
panya juu ya mifano hiyo. Ikisha anaweza kuona uhusiano baina ya
aina za maneno na maneno ya mifano yenyewe. Sifa ya mifano hai ina
faida kubwa kwenye mazoezi vilevile: badala ya kupata majibu sahihi
moja kwa moja, mwanafunzi anaweza kujaribu tena akiwa amekosea, na
anaweza kupata madokezo akikwama. Vilevile, mwishoni mwa kila zoezi
atapata matokeo ya utendaji wake, ambayo yatamsaidia kujipima
mwenyewe, na yatamsaidia mwalimu kuwapima wanafunzi wake. |
| 3) |
Sehemu ya tatu ya manufaa ya CD ni uwezekano wa kuunganisha
sehemu mbalimbali kwa njia ya link'. Hii inatupa nafasi
kuchangia maarifa ya ziada bila ya kufumba maelezo ya msingi. Kwa
mfano: kwenye maelezo ya ngeli tunaweza kuunganisha makala kuhusu
semantiki ya ngeli, kuhusu ushiriki wa maneno ya mkopo kwenye
utaratibu wa ngeli, na vinginevyo. Mwanafunzi anaweza kuyasoma
makala haya kwa hisani yake, na baada ya mzunguko atarudi moja kwa
moja kwenye barabara kuu, yaani maelezo ya msingi, bila ya kupotea
kwenye wingi wa maarifa. Vilevile, michango ya ziada siyo lazima
iwemo kwenye CD yenyewe; hata makala ambazo zimo kwenye mtandao
zinaweza kuunganishwa na kozi kwa njia ya link'. Hatujapata
nafasi kutia makala ambazo ziko nje ya kozi, kwa hivo itabidi
niwaonyeshe links' zinavyofanya kazi kwenye utaratibu
mwingine tunaoutumia: <U01maz-e53.html> Mwishoni mwa kila
sehemu kuna muhtasari ya maelezo maalum ya sehemu hiyo. Kwa kutumia
njia ya links' kwenye muhtasari hizo tunampa nafasi
mwanafunzi kuzitizama tena sehemu ambazo hajazifahamu. |
Hizo ndizo faida kuu za CD kulinganisha na kitabu.
Juu ya hayo, kuna faida kadhaa za masomo ya CD kulinganisha na
masomo ya uso kwa uso, yaani darasani. Nitazitaja mbili:
| 1) |
Faida ya kwanza ni kwamba anayeamua kasi ya masomo si mwalimu,
bali ni mwanafunzi mwenyewe; yaani ikiwa mwanafunzi hajafahamu
sehemu moja ya maelezo, anaweza akasimama hapohapo kuyachunguza
zaidi hayo maelezo na mifano yake. Anaweza hata akarejea na kupata
maelezo zaidi kwa njia ya links', mpaka afahamu. Darasani
haiwezekani kumjaalia kila mwanafunzi kwa kuwa kila mwanafunzi ana
ufahamu wake. |
| 2) |
Faida ya pili, ambayo inatokana na faida ya kwanza, ni kwamba
wanafunzi wa vyeo mbalimbali wanaweza kufundishwa kwa kutumia CD
hiyo moja. Kwa mfano, kwenye kozi, maelezo ya sarufi yanaweza
kutungwa kwenye lugha rahisi, bila ya kutumia istilahi au dhana
nyingi za isimu. Hivo hata mtu ambaye si mtaalamu wa lugha anaweza
kuyafahamu masomo na anaweza kuyatumia kujifunza lugha hiyo. Na
wakati huohuo tunaweza kumridhisha mwanaisimu: yeye atakuwa na
nafasi kufuata njia nyingine kwenye kozi hiyo hiyo, kwa kutumia
utaratibu wa link'. Darasani haiwezekani kufuata njia mbili
hizi; kila ukichukua kikundi kimoja cha wanafunzi, utakiacha
kingine. |
Kwa kusema hivyo basi, sina maana kuwa masomo ya CD, yanavyopangwa
kwenye ALI Swahili, yanakusudiwa kuchukua nafasi ya masomo
darasani. Hatukusudii kompyuta kuchukua nafasi ya mwalimu, wala
hiyo haiwezekani. Ukiacha faida ambazo nimekwisha kuzitaja, zipo
kasoro mbalimbali za kujisomea mwenyewe, tukilinganisha na
utaratibu wa kufundishwa darasani. Nitazitaja kasoro tatu ambazo
zote zinatokea endapo mwanafunzi atajisomea mwenyewe bila ya
mwalimu:
| 1) |
Hata ikiwa mifano hai itarahisisha ufahamu, mara nyingi
mwanafunzi atakuwa na maswali ambayo lazima ajibiwe kabla hajaweza
kufahamu maelezo kwa ufahamu wake. Na maswali hayo hayatajibika kwa
kompyuta. Mtungaji wa masomo, kwa uzoefu wake wa kufundisha,
anaweza akajua baadhi ya maswali ambayo yataulizwa, na anaweza
kuyaingiza kwenye maelezo yake; lakini hawezi kuyajua maswali yote.
Hapo itakuwa lazima kuwa na mwalimu ambaye atajibu maswali na
kuwasaidia wanafunzi ana kwa ana. |
| 2) |
Kasoro ya pili inahusu matamshi. Kwa kutumia sauti kwenye
masomo, tunampa mwanafunzi nafasi kufananisha matamshi yake na
matamshi ya mzungumzaji wa asili. Hivyo anaweza kurekebisha
matamshi kwa uamuzi wake yeye. Lakini uamuzi huo unaweza kuwa
tafauti na uamuzi wa mzungumzaji wa asili anaposikia matamshi hayo;
yaani mwanafunzi anaweza akakosea ki-matamshi bila yeye mwenyewe
kutambua. Kwa hivyo itakuwa lazima akutane na mzungumzaji wa asili,
au mtu mwenye uzoefu wa kuzungumza lugha hiyo, arekebishwe matamshi
yake. |
| 3) |
Kasoro kubwa ya tatu ni kwamba kompyuta haiwezi kumzungumzisha
mwanafunzi; yaani hata ikiwa nafasi zipo kwa mwanafunzi kutumia
ujuzi wake ki-bunifu, kwa kutunga sentensi mwenyewe au kuchangia
kwenye mazungumzo, hakuna uhakika kwamba kweli atazitumia nafasi
hizo. Kwa uzoefu wangu wa kufundisha najua kwamba kuna tafauti
kubwa baina ya kujifunza lugha na kusema lugha; mara nyingi
mwanafunzi anajua lugha kinadharia, lakini anashindwa kuchangia
kwenye mazungumzo kwa sababu anaona haya kutumia lugha
anayojifunza. Haya hiyo inaweza kupunguzwa darasani tu, kwa
kumlazimisha mwanafunzi azungumze tangu mwanzoni. |
Tukishajua faida na kasoro za vifaa vya kompyuta kwenye kufundisha
lugha, itabidi tuviunganishe na taratibu za awali kwa namna ambayo
inaongeza faida na kupunguza kasoro za kila chombo. Kutokana na nia
hiyo, katika mradi huo wa ALI Swahili masomo yatapangwa
kwenye sura tatu, ambazo zitaingiliana:
| 1) |
Masomo ya nafsi kwa kutumia CD. Maelezo mengi mwanafunzi
atajisomea mwenyewe, kwa mwendo wake, kwa kufuata masomo ya CD na
makala ya ziada. Atapewa ratiba ambapo amepangiliwa hatua zake,
yaani muda anaoweza kuutumia kwa kila somo. |
| 2) |
Madarasa ya mtandao'. Licha ya kujisomea mwenyewe,
mwanafunzi atapewa nafasi kuwasiliana na wanafunzi wenzake na
mwalimu. Nafasi hii itatumia vifaa vya mtandao, hasa barua za umeme
na chumba cha mazungumzo', yaani chat room'. Vifaa
hivyo vitaongozwa na mwalimu: yeye atatoa mazoezi au mada ambazo
zitazungumzwa kwenye chat room', na atajibu maswali ambayo
yatamfikia kwa barua za umeme. Ikitakiwa, mwanafunzi anaweza kupewa
wakati au muda maalum ambapo lazima awemo kwenye mtandao;
teknolojia za kompyuta zinamwezesha mwalimu hata kukagua kama
mwanafunzi anatimiza wajibu huo. |
| 3) |
Madarasa ya uso kwa uso'. Baadhi ya wakati mwalimu
atakutana na wanafunzi wake darasani kama kawaida. Lakini yaliyomo
ya madarasa yatabadilika. Kwa sababu mwanafunzi atakuwa
ameshajisomea maelezo mengi kwa kutumia CD, mwalimu atakuwa na
nafasi ya kufundisha mengine badala yake. Hapo itakuwa vizuri
kusisitiza vipengele ambavyo ni vigumu kufundishwa kwa njia ya CD:
kwa mfano matamshi, mazungumzo, ufahamu wa kusikiliza, na
kadhalika. Vilevile, kutokana na mawasiliano kwenye mtandao,
mwalimu atajua baadhi ya matatizo waliyo nayo wanafunzi, na ataweza
kupanga masomo darasani kulingana na matatizo hayo. Na muda
ukibaki, anaweza kuzungumzia baadhi ya matini kwa undani
zaidi. |
Mpangilio huo unaonyesha kwamba vifaa vya kompyuta, vilivyotajwa
kwenye maelezo yangu, hayakusudiwi kuchukua nafasi ya mwalimu.
Lakini itabidi mwalimu abadilishe utaratibu wake wa kufundisha:
badala ya kutayarisha masomo ya sarufi, ya kufundishwa darasani,
kazi yake kubwa itakuwa kuwasiliana na wanafunzi kwa njia ya
mtandao, ambapo atawapa mazoezi na kuyasahahisha, pamoja na kujibu
maswali ya wanafunzi. Vilevile, mwalimu atatakiwa awe na uwezo wa
kubadilisha mipangilio ya mafunzo kulinganisha na mahitaji ya
wanafunzi. Mahitaji hayo yatajulikana kutokana na mawasiliano
mtandaoni.
Bila ya shaka hii itaongeza kazi yetu sisi walimu. Lakini vilevile,
itaifanya kazi hiyo iwe ya kuvutia zaidi, kwa sababu itakuwa na
sura mbalimbali. Na nina uhakika kwamba ikiwa nia yetu ni
kufundisha lugha kama jambo hai, kama chombo cha uhusiano baina ya
watu, basi vifaa vya kompyuta vitatuzalia matunda mengi katika kazi
hiyo.
Kuwepo kwa kompyuta kwenye sehemu mbalimbali za maisha ya kila siku
si swala la upendo, bali ni swala la lazima na la uhakika siku
hizi. Kwa hivo tusifumbie macho jambo hili, bali tulichunguze na
kulitumia ipasavyo ili kufaidisha malengo ya kazi yetu.
|